Search This Blog

Thursday, December 22, 2011

KIKOSI CHA MASTAA WA BONGO WALIOCHEMSHA KABLA YA WAKATI…..

KATIKA kipindi cha miaka kumi iliyopita, nchi yetu (Tanzania) imebahatika kutoa wachezaji mahiri katika ukanda wetu
Mbarouk Suleiman Mbarouk
Wakati kizazi cha magolikipa mahiri kama, Mohammed Mwameja, Steven Nemes, Denis Edwin, Peter Manyika na Ismail Suma kikiishia, kulikuwa na makipa wengi vijana, Juma Kaseja, Mengi Matunda, Noel Pompi, Farook Ramadhani na wengineo, lakini kila mmoja alikuwa anaangalia ni hadi wapi vipaji vya makipa hao vingefika. Mbarouk Suleiman alikuwa ni mmoja ya makipa bora nchi kutokea Visiwani Zanzibar, lakini kutua kwake Yanga mapema mwaka 2006 ilikuwa ni sawa na kuupa kisogo mchezo wa soka akiwa na umri mdogo.

Said Sued
Kijana huyu wa Ilala alikuwa ni mchezaji mdogo zaidi katika ligi kuu ya Bara. Sued alijiunga na Simba mwaka 2001 akiwa kidato cha pili, na ndiyo kwanza alikuwa na umri wa miaka 17 kwa karibu alifuatiwa na Nico Nyagawa aliyekuwa Mtibwa Sugar wakati huo. Sued alikuwa anapanda kama mlinzi wa zamani wa Italia, Christian Pannucci, alikuwa mpigaji mzuri wa mipira iliyokufa kama Deniss Irwin, na mfungaji wa magoli ya mbali kwa staili ya Sergio Ramos. Matatizo ya mara kwa mara ya kinidhamu inasemekana ndiyo sababu kubwa ya Sued kutengwa na soka na kumuacha kinda mwezake wa mwaka 2001, Nyagawa akivaa beji ya unahodha wa Simba.

Twaha Abubakar ‘Abdul Mtiro’
Itikadi ya Usimba na Uyanga imemaliza kipaji cha Mtiro. Inasemekana kuwa mara baada ya kupaisha penati ya mwisho katika fainali ya ligi kuu ndogo mwaka 2007 mjini Morogoro, wakati timu yake ya Yanga ikicheza na mahasimu wao Simba, moja kwa moja aliwatumbukia ‘nyongo’ wana Yanga wote. Lakini ukiangalia kwa makini namna wanavyocheza ‘mafullback’ wa kushoto wa sasa wa Stars unaweza kuona kuwa Mtiro angeweza kuhodhi namba hiyo.

Boniface Pawassa
Kila alipokuwa anatema mate mshambuliaji mahiri wa zamani wa Misri, Hossam Hassan basi Pawassa alikuwa anayakanyaga, achana na stori kuwa Cannavaro anakaba sana, kwa Pawassa hakika usingeweza kumfikiria Cannavaro. Utovu wa nidhamu inasadikiwa ni sababu kubwa ya Pawassa kumaliza kipindi chake cha uchezaji akiwa na umri mdogo.


Hamis Yusuf.
Waziri wa ulinzi’ aliyehukumiwa na ubora wa Mamadou Niang. Ndiyo kabla ya Stars haijakwenda jijini Dakar kila mmoja alikuwa anafikiria ni nani na nani wangeanza katika kikosi cha kwanza (katika nafasi ya ulinzi wa kati), Victor Costa, Salum Sued na Yusuph wote walikuwa katika kiwango cha juu. Ilikuwa ni siku mbaya kwa Yusuph kwani hakuonekana kama ni kweli yeye ni ‘waziri wa ulinzi’ Sasa yupo AFC lakini ni sawa na kusema kuwa Yusuph ni moja ya vipaji vinavyotoweka kabla ya muda.


Waziri Mahadhi ‘Mendieta’
Katika umri wa miaka kati ya 28-30 aliyonayo sasa ni kichekesho kusema kuwa kiungo huyu mahiri wa zamani wa Stars ni kocha!! Mendieta kama alivyokuwa akitambulika kwa mashabiki wa soka nchini kutokana na kufananishwa na kiungo wa zamani wa Hispania, Gaizka Mendieta. Inasemekana kuwa majeruhi ya mara kwa mara yamemaliza makali ya kiungo huyu na kuchangia kwa kiasi kikubwa kujiweka kando na soka.

Shekhan Rashid Abdalah
Anavutia mabinti wengi kutokana na muonekano wake, upole wake lakini kikubwa ni namna anavyoupendezesha mchezo wa soka. Mara baada ya kutoroka katika klabu ya Simba mwaka 2003 na kwenda Norway, Shekhan aliporudi tena nchini mwaka mwaka 2004 hakuwa yule aliyepiga penati katika maji dhidi ya Ismailia ya Misri mwaka 2001. Mechi moja tu ilitosha kumuelezea kiungo huyu kuwa hana jipya tena, ni wakati Simba ilipocheza na Zanaco ya Zambia mwaka 2004. Alijitahidi kurejea katika kiwango chake lakini alivunjika mguu mwaka 2007, inasemekana kwa sasa yuko nchi Sweden.





Christopher Alex Massawe
Kama ilivyo kwa Shekhan, Alex pia alikuwa na mvuto kwa kina dada waliokuwa wakienda kutazama mechi za Simba au Stars.Alikuwa ana uwezo mkubwa wa kucheza kama mlinzi au kiungo mshambuliaji. Kisa cha Mchaga huyu kuachana na soka akiwa na miaka chini ya 28, inasemekana kuwa alipata mwanamke wa kizungu ambaye hakutaka acheze soka, ndiyo maana alikuwa anafanya vituko vingi katika siku zake za mwisho akiwa na Simba.

Abuu Ramadhani ‘Amokachi’
Mshambuliaji Mfungaji wa zamani wa Yanga, Abuu alikuwa ni mmoja wa washambuliaji wenye rekodi nzuri ya ufungaji katika Tanzania. Sijui alikutwa na nini na kutibuana na viongozi wa zamani wa klabu yake ya Yanga. Kasi, uwezo wa kupiga mashuti ni baadhi ya sifa za mshambuliaji huyu wa zamani wa Stars. Wapo wanaosema kuwa majeruhi yamepoteza makali ya kijana huyu.

Aaron Nyanda
Namna anavyocheza Nurdin Bakari kwa sasa ndivyo alivyokuwa anacheza Nyanda. Ni kiraka aliyekuwa na uwezo wa kucheza mahali popote uwanjani, lakini daima alikuwa anavutia akicheza namba 10 au 11, kwani ungeweza kuona vionjo ambavyo si rahisi kuviona kwa Nurdin Bakari. Inasemekana majeruhi na masomo yalimfanya kuachana na soka la ushindani akiwa na umri mdogo.

4 comments:

  1. kuna jembe Yusuph Soka, ci dhani kama 22 kafika, sasa atujui alipo potelea

    ReplyDelete
  2. kaka hapo mimi namkumbuka sana shekhan rashid kiungo wa hatari,kweli mfumo wetu unavifanya vipaji vikubwa kama hivi vipotee na visifikie potentilities zake

    ReplyDelete
  3. sijui waliuchukuliaje mpira ..maana kama ndio ingekuwa maisha sidhani sababu hizo zinatosha kwa wao kupoteza nafasi yao hiyo...

    Poor them..

    classic

    ReplyDelete
  4. shaffih siamini kama umemsahau DANNY PANJU! alilinda goli za Azania sekondari kwa umakini mkubwa, akasajiliwa na simba akiwa na mvuto mkubwa, bahati mbaya katika siku zake za mwanzo akakutana na mechi ngumu ya simba na yanga na nakumbuka simba ikafungwa yeye akiwa golini msala ukamuangukia.. jamaa hakutamani tena kucheza soka na sijui yupo wapi tena PANJU!

    ReplyDelete