Search This Blog

Thursday, October 13, 2011

YANGA WAKIRI KUFULIA, WAMPIGIA MAGOTI MANJI NA KUTOA SALAMU ZA BIRTHDAY


Kutokana na hali ya kifedha kuzidi kuwa ngumu, uongozi wa Klabu ya Yanga chini ya mwenyekiti wake Lloyd Nchunga umemwangukia aliyekuwa mfadhili na mdhamini wao, Yusuf Manji, ili aweze kurejea kuokoa jahazi.


Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Yanga, Lloyd Nchunga, alisema kuwa wamefikia uamuzi wa kumsihi Manji arejeshe ufadhili na udhamini baada ya mambo kuanza kwenda mrama.


Nchunga alisema baada ya uongozi kuona wameshindwa kumpata mfadhili wa kuchukua nafasi ya Manji, ambaye alijiondoa kudhamini na kuifadhili Yanga na kubaki mwanachama wa kawaida, waliona ni vema kumuomba arudi.

“Baada ya kutafakari kwa kina, tuliona tuna kila sababu ya kumsihi na kumwomba Manji arejee na napenda kuwaambia kuwa tumekuwa na majadiliano ya muda mrefu na ndugu Yusuf Manji na kimsingi amekubali,” alisema Nchunga.


Alifafanua kuwa baada ya uongozi kumwandikia barua rasmi Manji, kumuomba arejee kuidhamini, mfanyabiashara huyo aliomba muda wa kutafakari ili aweze kujadiliana na familia yake, pamoja na wafanyabiashara wenzake kabla ya kuridhia.


Aliongeza kuwa Manji amesema kabla ya kutoa uamuzi wa ama kurudi ama kutorudi, ameomba kwanza kukutana na Kamati ya Utendaji na baada ya mazungumzo hayo, ndipo atafikia uamuzi wa mwisho juu ya maombi hayo.

“Pia nichukue fursa hii kwa niaba ya Yanga, kumtakia ‘birthday’ siku njema ya kuzaliwa ndugu yetu Manji, ambaye kwa sasa yupo nchini Marekani na anatarajia kurudi nchini Ijumaa, huku akiwa katika kusherehekea siku yake ya kuzaliwa, kwani alizaliwa Oktoba 14, pia tujitokeze kumpokea siku atakaporudi,” alisema Nchunga.

No comments:

Post a Comment