Search This Blog

Saturday, September 24, 2011

TFF MABINGWA WA KUVUNJA KANUNI LIGI KUU BARA


Pamoja na kuonekana likifuatilia kwa karibu utekelezwaji wa kanuni zake ndogo ndogo katika uendeshaji wa Ligi Kuu msimu huu, blog hii imebaini bado kuna kanuni za msingi ambazo chombo hicho kimekuwa kikizipuuza licha ya kuwa imezitunga yenyewe.

Moja ya kanuni hizo za msingi ambazo TFF imeshindwa kuitekeleza ni pamoja na ile ya 12 inayozungumzia bima.
Kipengele cha kwanza cha kanuni hii kinasema kuwa viongozi na wachezaji wote lazima wawekewe bima na klabu zao na kuongeza kuwa klabu itakayokiuka kanuni hiyo haitashirikishwa katika michuano yoyote inayosimamiwa na TFF.

Aidha kipengele cha pili cha kanuni hiyo kinatoa maagizo kwa Chama cha Walimu wa Mpira wa Miguu (TAFCA) kuhakikisha wanachama wake wanawekewa Bima na klabu husika.Pia Chama cha Madaktari wa Michezo Tanzania (TASMA) na wenyewe wanatakiwa kuhakikisha kwamba wanachama wake wanawekewa bima na klabu husika.

Hata hivyo licha ya TFF kusisitiza utekelezwaji wa kanuni hiyo, uchunguzi iliofanywa na blog hii baada ya kufanya mahojiano na baadhi ya wachezaji na viongozi wa klabu 14 zinazoshiriki Ligi Kuu umebaini kuwa kanuni hiyo haitekelezwi kwa asilimia 100 kanuni na bado klabu zinaendelea kushiriki Ligi Kuu kama kawaida bila hatua zozote kuchukuliwa na shirikisho hilo.

Mchezaji mmoja wa safu ya ushambuliaji ya Yanga mbali ya kukiri kutokuwa na bima pia alisema hajawahi kusikia suala hilo likizungumziwa katika klabu yake.

Msemaji wa klabu ya African Lyon, Sherally Abdallah alizungumzia suala hilo kwa kusema kuwa wachezaji waliokatiwa bima ni wale waliosajiliwa misimu ya nyuma, lakini kwa wale wa msimu huu bado suala lao linashughulikiwa.

Ofisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania TFF, Boniface Wambura baada ya kuulizwa ni kwa nini shirikisho lake limeshindwa kusimamia kanuni ilizozitunga lenyewe badala ya kutoa majibu yeye alimtaka mwandishi wa habari hii aziulize klabu ni kwa nini zimeshindwa kutekeleza kanuni hiyo na baada ya hapo ndio atafutwe yeye.

Source:Mwananchi.co.tz

No comments:

Post a Comment