Search This Blog

Thursday, September 29, 2011

SALUM MACHAKU AONDOLEWA POP, SUNZU KURUDI DIMBANI


SIMBA imepata matumaini ya kuendelea kufanya vema katika Ligi Kuu soka Tanzania Bara, baada ya nyota wake waliokuwa majeruhi akiwemo kiungo mshambuliaji, Salum Machaku, kutolewa plasta ngumu (POP).

Machaku aliwekewa POP baada ya kuumia alipokuwa na timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ ilipokuwa inajiandaa na mchezo wa kuwania kufuzu ushiriki wa Kombe la Mataifa ya Afrika dhidi ya Algeria.

Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alisema jana kwamba baada ya Machaku kutolewa POP juzi, tayari ameanza mazoezi mepesi kwa ajili ya kujiweka sawa na Ligi Kuu.

Alisema Machaku anaungana na Mwinyi Kazimoto, ambaye pia aliteguka mguu katika fainali za kuwania Kombe la Kagame, michuano iliyofikia tamati Julai 10 katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Alisema kupona kwa wachezaji wake ni faraja kwani wana uhakika timu yao itaendelea kufanya vema katika ligi hiyo, ambao kwa sasa wanashikilia usukani kwa kuwa na pointi 18.

Kamwaga aliongeza kuwa, mshambuliaji wake Mzambia Felix Sunzu, ambaye alishonwa nyuzi nne usoni baada ya kuumia katika mchezo dhidi ya Toto Africa uliochezwa wiki iliyopita kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza, naye ameanza mazoezi.

Aliongeza kuwa wachezaji wa timu hiyo ambao wako katika mapumziko ya wiki moja, wanatarajiwa kuanza kujinoa keshokutwa kwa kuanza mazoezi mepesi.

Aidha, Kocha Mkuu, wa Simba, Moses Basena, aliyekwenda kwao kwa matatizo ya kifamilia anatarajiwa kurejea Oktoba mosi kwa ajili ya kuendelea na kazi yake.

No comments:

Post a Comment