Search This Blog

Thursday, September 29, 2011

KAMWAGA: PARTNERSHIP YA COSTA NA NYOSSO YAMCHOMESHA MAHINDI YONDANI.


Partnership iliyopo kati ya beki Victor Costa na Juma Nyoso ndiyo inayomnyima namba katika kikosi cha kwanza beki wa Simba, Kelvin Yondani na wala sio ana matatizo na uongozi wa klabu hiyo.

Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema kitu kinachomfanya mchezaji huyo kutokuonekana katika mechi za Simba hivi sasa ni kutokana na uelewano katika safu ya ulinzi ulioonyeshwa na Nyoso na Costa katika michezo yao yote waliyocheza.

''Hayo ni maamuzi ya kocha kumpanga au kutompanga, lakini safu ya ulinzi ni moja ya nafasi muhimu katika timu, unatakiwa ufanye maamuzi mazuri na makini katika upangaji, kocha kaona Costa na Nyoso wanaelewana zaidi kuliko wachezaji wengine katika nafasi hizo,'' alisema Kamwaga.

Alisema kwa mfano katika mechi yao dhidi ya Toto African ya Mwanza kocha alimpanga Obadia Mungusa na Costa, lakini walikuwa hawaelewani kabisa na kusababisha kuiachia safu ya ushambuliaji ya Toto kupita kilaini na kupata mabao matatu.

Kuhusiana na suala la mchezaji huyo kutoroka kambini, Kamwaga alisema kwa upande wao kama uongozi hawalijui hilo kwa kuwa wachezaji wao wote wamewaruhusu kwenda mapumziko makwao.

''Hatuwezi kujua kama katoroka au la kwa kuwa siku zote tulikuwa naye kasoro wakati tunaenda Kagera tulimuacha kwa kuwa tulienda na wachezaji ambao walikuwa wanacheza tu na tuliporudi hakulipoti kambini na baada ya mchezo wa Mtibwa tulivunja kambi,''alisema Kamwaga.

Hivi karibuni zilikuwapo taarifa za kutoroka kambini mchezaji huyo kwa madai kuwa hapangwi katika mechi kwa kuwa ana ugomvi na kocha wa Simba, Moses Basena pamoja na viongozi wake na hii itakuwa ni mara ya pili mchezaji huyo kutoweka katika timu hiyo.

Kamwaga alisema timu yao itaingia kambini Oktoba mosi kwa ajili ya mchezo wao dhidi ya African lyon Oktoba 16 Jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment